Wagombea Ubunge
wawili wa Mkoa wa Mtwara waliotoka vyama vya upinzani na kuhamia Chama cha
Mapinduzi (CCM) wameeleza machungu waliyokuwa wakikumbana nayo wakati wakitaka
kuwatumikia wananchi wao.
Wabunge hao Bw. Cecil
Mwambe (Ndanda) na Bw. Katani Ahmed Katani (Tandahimba) ambao wamehamia CCM
kwenye kinyang’anyiro hiki cha ubunge, wamewaonya wakazi wa Masasi wasifanye
makosa ya kuchagua wagombea wa upinzani kwani wataendelea kukosa maendeleo.
Wametoa wito huo jana
(Jumatano, Oktoba 21, 2020) kwenye mkutano wa kuwanadi wagombea ubunge na
udiwani wa CCM uliofanyika kwenye viwanja vya Sabasaba kata ya Mkuti, wilayani
Masasi, mkoani Mtwara ambako Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa
ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa alikuwa mgeni rasmi.
Bw. Mwambe
anayegombea Ndanda na ambaye alihamia CCM akitokea Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (CHADEMA), alisema licha ya kuwa alikuwa akitamani wananchi wake
wapate huduma muhimu kama maji, afya na barabara, haikuwa rahisi kwake
kuchangia bajeti ya maendeleo kwa sababu walikuwa wanakatazwa.
“Mambo yaliyokuwa
yanafanyika huku Masasi hata sisi kule Ndanda tulikuwa tunayatamani. Hii ni kwa
sababu hakuna cha maana kule kilichoandikwa kwa ajili yenu, na mimi ni shahidi.
Katika miaka mitano ya ubunge wangu, sijawahi kuitikia NDIYO na madhara yake nimeyaona.
Ninawaomba sana, msifanye makosa hayo,” alisema.
Naye Bw. Katani
anayegombea Tandahimba na ambaye alihamia CCM akitokea Chama cha Wananchi
(CUF), aliwataka wananchi hao wasifanye makosa kwa sababu kule alikokuwa hawana
ilani.
“Kama Katani
anayeongea hapa mbele yenu, alikuwa Mwenyekiti wa Vijana Taifa na kaikimbia
CUF, wewe ni nani mwananchi wa Masasi hata upinge maendeleo ya nchi hii? Tena
niwaambie, kule hakuna ilani. Nawaomba wana Masasi msifanye makosa ya kuchagua
wagombea wa upinzani, sisi wenzenu tumeyaona tukiwa Bungeni.”
“Ukienda Bungeni
kutaka kusema Masasi tuna shida ya umeme, wakubwa wanasema kapinge bajeti.
Tutaupataje umeme? Tumekwenda Bungeni tumepiga plasta, sasa ukitaka kuomba
umeme, utaongea vipi na wewe midomo umeifunga plasta?”
“Wana Masasi
msitucheleweshe, hii gari ya Dkt. Magufuli inatelemka kwa kasi kuleta maendeleo
huku mikoa ya Kusini. Acheni Geofrey Mwambe awe mbunge wa jimbo la Masasi,
alete maendeleo,” alisisitiza.
Wakati huohuo,
mwanasiasa mkongwe na Waziri Mstaafu, Mama Anna Abdallah alisema anashangazwa
na tabia ya mgombea urais ambaye anatangaza kwamba ndoa za jinsia moja ni haki
ya msingi ya wananchi.
“Yuko mgombea wa
urais ambaye yeye anasema haonei aibu ushoga eti anauunga mkono. Yaani mwanaume
amuoe mwanaume mwenzake na mwanamke amuoe mwanamke mwenzake.”
“Anasema eti ni haki
za binadamu. Hivi kama baba yake angemuoa mwanaume mwenzake au mama yake
angeolewa na mwanamke mwenzake, yeye leo angekuwepo na angekuja kugombea
urais?”
“Rais wa namna hiyo
ana mawazo ya kishetani, hakuna dini hata moja inayosema juu ya ushoga. Hata
wanaogombea kwa kupitia chama hicho ninaanza kuwatilia shaka. Hakuna ushoga
katika nchi hii, hatutakiii! Haiwezekani, sisi tulioko hapa tumezaliwa na sisi
tumezaa. Watoto wetu waache kuzaa kwa ajili ya mtu mmoja anayesema hiyo ndiyo
haki. Hakuna haki kwenye ushoga, ni dhambi,” alisisitiza.
Mapema, aliyekuwa
mbunge wa jimbo la Masasi, Bw. Rashid Chuachua alisema katika wilaya hiyo,
ndani ya miaka mitano, waliwezaa kujenga madarasa 108 ya shule za sekondari na
mengine 355 ya shule za misngi.
Alisema kiasi cha sh.
bilioni 3.5 kilitolewa kwa ajili ya elimumsingi bila malipo huku sekta ya afya
ikiboreshwa kwa kujenga kituo cha afya cha Mbonde kwa gharama ya sh. milioni
500 na hospitali ya Mkomaindo ikipatiwa jengo la upasuaji lililogharimu sh.
milioni 228.
“Mradi wa maji
unaendelea kujengwa na ukikamilika, hatutakuwa na shida kabisa ya maji hapa
Masasi,” alisema na kuwaombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dkt. John
Pombe Magufuli, mgombea ubunge wa jimbo la Masasi, Bw. Geofrey Mwambe; na
wagombea udiwani 14 wa CCM wa jimbo la Masasi.