Matokeo chanyA+ online




Tuesday, March 17, 2020

KAMATI YA BUNGE YAPONGEZA HATUA ZILIZOCHOKULIWA NA SERIKALI KUKAMILISHA MRADI WA KINYEREZI I EXTENSION

Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (kulia), akiwaongoza Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, kutembelea Mradi wa Umeme wa Kinyerezi I Extension, Machi 16, 2020. Kulia kwa Waziri ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Dunstan Kitandula.
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeipongeza Serikali kupitia Wizara ya Nishati, kwa hatua ilizochukua katika kuhakikisha Mradi wa umeme wa Kinyerezi I Extension (megawati 185) unakamilika mapema iwezekanavyo.
Mwenyekiti wa Kamati, Dunstan Kitandula alitoa pongezi hizo mbele ya waandishi wa habari, wakati akizungumzia msimamo wa Kamati hiyo baada ya kutembelea Mradi husika uliopo eneo la Kinyerezi jijini Dar es Salaam, Machi 16, 2020.
 
Sehemu ya mitambo iliyopo katika Mradi wa Umeme wa Kinyerezi I Extension jijini Dar es Salaam. Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini (hawapo pichani), walitembelea Mradi huo, Machi 16 mwaka huu.
Alisema, Kamati iliamua kutembelea Mradi huo ili kujiridhisha kuhusu hatua zilizochukuliwa na Serikali baada ya kupata taarifa kwamba Mkandarasi aliyekuwa akitekeleza Mradi husika ambaye ni Kampuni ya Jacobsen Electro AS kutoka Norway,  amefilisika hivyo haendelei tena na kazi.
Akieleza zaidi, Kitandula alisema, Kamati ilitaka kujiridhisha kwamba kufilisika kwa Mkandarasi hakuiingizi nchi kwenye migogoro ya kimkataba inayosababisha Taifa kuingia gharama zaidi, lakini pia kujionea hatua zilizochukuliwa katika kuhakikisha Mradi unatekelezwa.

Meneja wa Mradi wa Umeme wa Kinyerezi I Extension, Mhandisi Abdallah Chikoyo (kulia), akitoa maelezo kuhusu Mradi huo kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, walipotembelea eneo hilo, Machi 16, 2020. Wa tatu kutoka kulia ni Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani na kulia kwake ni Mwenyekiti wa Kamati husika, Dunstan Kitandula.“Kusema kweli sisi kama Kamati tumeridhishwa sana na hatua zilizochukuliwa kuhusiana na suala hili, hivyo kwa niaba ya Kamati nitumie nafasi hii kuipongeza Serikali.”Katika hatua nyingine, Kamati imekiri kuridhishwa na kufurahishwa na uhakika uliotolewa na Serikali kuwa umeme kwa ajili ya matumizi ya Treni ya mwendokasi (SGR) pindi itakapokamilika upo tayari na kwamba hauhusiani na kukamilika au kutokamilika kwa Mradi huo wa upanuzi wa Kinyerezi I. 

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Dunstan Kitandula (mbele) na Wajumbe wa Kamati hiyo, wakikagua Mradi wa Umeme wa Kinyerezi I Extension, Machi 16, 2020.

Kuhusu suala la malipo kwa wakandarasi wa ndani waliokuwa wamepewa mkataba na mwekezaji husika ambaye amefilisika, Kitandula alibainisha kuwa Kamati yake imejiridhisha na maelezo yaliyotolewa na Serikali kuwa mchakato unaohusisha kuainisha mchanganuo wa malipo hayo, uko katika hatua za mwisho ili waanze kulipwa.
Awali, akiwasilisha taarifa fupi ya Mradi kwa Kamati husika, Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani alisema hatua zilizochukuliwa na Serikali katika kuhakikisha nchi haipati hasara baada ya Mkandarasi kufilisika ni pamoja na kuhakikisha vifaa vyote vinavyohusika katika utekelezaji wa mradi viko katika eneo hilo.
Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani akiwasilisha maelezo mafupi ya utekelezaji wa Mradi wa Umeme wa Kinyerezi I Extension kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, baada ya kutembelea Mradi huo Machi 16, 2020 jijini Dar es Salaam.
Aidha, alibainisha kuwa Serikali ilijiridhisha kuwa malipo yaliyofanyika kwa Mkandarasi huyo ni yale tu yanayoendana na kiwango cha kazi aliyofanya na siyo zaidi.
“Mkandarasi amekamilisha kazi kwa wastani wa takribani asilimia 85 na amelipwa kwa kazi ya asilimia 68 hivyo hakuna hasara,” alifafanua Waziri.
Aliongeza kuwa, Serikali kwa kushirikiana na taasisi nyingine mbalimbali ikiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, imejipanga kuhakikisha kazi iliyobaki, ambayo ni takribani asilimia 14, inakamilika ndani ya kipindi kisichozidi mwezi Desemba mwaka huu.
 



Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, wakikagua Mradi wa Umeme wa Kinyerezi I Extension uliopo jijini Dar es Salaam, Machi 16, 2020.
“Nimeshatoa maelekezo kwa wataalamu kutoka taasisi zote zinazohusika kuhakikisha tunampata Mkandarasi mwingine ndani ya siku 30 zijazo ili aanze kazi mara moja na kukamilisha kabla ya Desemba.”
Akieleza zaidi, Dkt Kalemani alisema Serikali imedhamiria kumpata Mkandarasi mwenye uwezo ambaye gharama yake haitazidi mpango mahsusi wa gharama halisi ya mradi.
Naye Meneja wa Mradi huo, Mhandisi Abdallah Chikoyo, aliwaeleza Wajumbe wa Kamati kuwa, jumla ya miradi saba ya umeme unaotokana na gesi imepangwa kutekelezwa na Serikali.

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, wakikagua Mradi wa Umeme wa Kinyerezi I Extension uliopo jijini Dar es Salaam, Machi 16, 2020.

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, wakikagua Mradi wa Umeme wa Kinyerezi I Extension uliopo jijini Dar es Salaam, Machi 16, 2020.

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, wakikagua Mradi wa Umeme wa Kinyerezi I Extension uliopo jijini Dar es Salaam, Machi 16, 2020.

Aliitaja miradi hiyo kuwa ni pamoja na wa Kinyerezi I (megawati 150) ambao ulikamilika mwaka 2016, Kinyerezi I Extension (megawati 185) ambao ndiyo uliotembelewa na Kamati na uko katika hatua za mwisho kukamilika pamoja na Kinyerezi II (megawati 148) uliokamilika mwaka 1918.
Mwingine ni Mradi wa Kinyerezi III utakaotekelezwa kwa awamu mbili huku kila awamu ikitarajiwa kuzalisha megawati 300. Utekelezaji wake uko katika hatua za kukamilisha utafiti na upembuzi yakinifu ili uanze kutekelezwa.
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, wakikagua Mradi wa Umeme wa Kinyerezi I Extension uliopo jijini Dar es Salaam, Machi 16, 2020.


Veronica Simba – Dar es Salaam

Mhandisi Chikoyo alitaja miradi mingine kuwa ni Kinyerezi IV (megawati 430), Mradi wa Mtwara (megawati 300) pamoja na Mradi wa Somanga Fungu (megawati 350 hadi 370).
Mradi wa Kinyerezi I Extension unagharamiwa na Serikali ya Tanzania kwa asilimia 100 na gharama yake ni Dola za Marekani milioni 188 sawa na shilingi za Tanzania takribani 435.48.

No comments:

Post a Comment