Matokeo chanyA+ online




Wednesday, August 14, 2024

RAIS DK. MWINYI; ZANZIBAR KUPUNGUZIWA GHARAMA ZA UENDESHAJI WA MIRADI

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dk. Hussein Ali Mwinyi, ameonesha utayari wa Serikali ya Zanzibar kushirikiana na Taasisi ya Mabenki Yasiyo na Mipaka (Bankers without Boundaries) katika kuwekeza kwenye miradi ya kipaumbele ambayo italeta tija kwa nchi.

Dk. Mwinyi alitoa kauli hiyo leo, tarehe 14 Agosti 2024, alipokutana na Mkuu wa Taasisi hiyo, Bw. Matteo Scollabrino, aliyefika Ikulu Zanzibar akiwa ameongozana na ujumbe wake kutoka makao makuu ya taasisi hiyo yaliyopo nchini Uingereza.

Rais Dk. Mwinyi alieleza kuwa Serikali inatilia mkazo sekta muhimu kama Uchumi wa Buluu, Kilimo, Nishati, Miundombinu, na Afya. Sekta hizi zimebainishwa kuwa ni kipaumbele na zinahitaji msukumo wa ziada ili kuhakikisha zinaweza kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa Zanzibar.

Kwa upande wake, Bw. Scollabrino alieleza kuwa Taasisi ya Bankers Without Boundaries, ambayo inafanya kazi katika nchi 40 duniani, inalenga kushirikiana na Serikali ya Zanzibar kuwekeza katika miradi isiyo na athari kwa mazingira na inayopunguza gharama za uendeshaji. Aidha, alithibitisha kuwa taasisi hiyo imetenga kiasi cha Dola Milioni 500 kwa ajili ya kufanikisha malengo ya uwekezaji huo.

Kikao hicho muhimu kilifanyika Ikulu Zanzibar na kuhudhuriwa na watendaji wa Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango, pamoja na wawakilishi wa Presidential Delivery Bureau (PDB), ambao wana jukumu la kuhakikisha utekelezaji wa miradi hiyo unafanyika kwa ufanisi na manufaa kwa wananchi wa Zanzibar.

#Matokeo ChanyA+

No comments:

Post a Comment