Rais
 wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza
 na Wachezaji wa timu ya Taifa ya Mpira wa Miguu Taifa Stars ambao 
walifika Ikulu mara baada ya kufanikiwa kufuzu kushiriki Fainali za 
michuano ya Mataifa ya Africa AFCON baada ya kuifunga Timu ya Taifa ya 
Uganda The Cranes magoli 3-0 jijini Dar es Salaam.
 Wachezaji
 wa timu ya Taifa ya Mpira wa Miguu Taifa Stars waliopo upande wa kulia 
pamoja na viongozi wengine wakionesha ishara ya magoli matatu ambayo 
timu ya Taifa iliupata siku ya jumapili zidi ya Timu ya Taifa ya Uganda 
The Craines na kufanikiwa kufuzu kucheza Fainali za michuano ya Mataifa 
ya Africa AFCON nchini Misri baadae mwaka huu.
 Sehemu
 ya Wachezaji wa  wa timu ya Taifa ya Mpira wa Miguu Taifa Stars waliopo
 upande wa kulia pamoja na viongozi wengine wakiwa katika ukumbi wa 
Mkutano Ikulu jijini Dar es Salaam.
 
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Dkt. John Pombe Magufuli 
akisalimiana na mchezaji wa Timu ya Taifa Taifa Stars Shabani Iddi 
Chilunda mara baada ya kumaliza kuzungumza na wachezaji hao.
 Mwenyekiti
 wa Kamati ya Uhamasishaji ya Timu ya Taifa Stars ambaye ni Mkuu wa Mkoa
 wa Dar es Salaam Paul Makonda wanne kutoka kushoto waliokaa pamoja na 
wachezaji Wachezaji wa  wa timu ya Taifa ya Mpira wa Miguu Taifa Stars 
waliopo upande wa kulia pamoja na viongozi wengine wakiwa katika ukumbi 
wa Mkutano Ikulu jijini Dar es Salaam.
 Bondia
 wa Ngumi za kulipwa Hassan Mwakinyo kutoka Tanga akijitambulisha Ikulu 
jijini Dar es Salaam mara baada ya kupewa nafasi ya kuzungumza kuhusiana
 na mafanikio yake makubwa aliyoyapata katika ngumi za kulipwa pamoja na
 kuitangaza nchi kimataifa.
 Mfungaji wa goli la pili la Taifa Stars zidi ya Uganda Erasto Nyoni akijitambulisha Ikulu jijini Dar es Salaam.
  Bondia wa Ngumi za kulipwa Hassan Mwakinyo kutoka Tanga akizungumza mara baada ya kupewa nafasi Ikulu jijini Dar es Salaam.
 Rais
 wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akipiga 
makofi wakati Bondia Hassan Mwakinyo alipokuwa akizungumza.
 Mchezaji
 wa Timu ya Taifa ya Tanzania Taifa Stars Jonas Mkude akifurahia jambo 
wakati wakiwa Ikulu jijini Dar es Salaam pamoja na wachezaji wenzake.
 Rais
 wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli 
akisalimiana na Kocha wa Taifa Stars Emanuel Amunike mara baada ya 
kumaliza kuzungumza na wachezaji wa Timu ya Taifa.
 Rais
 wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli 
akimsikiliza Mchezaji wa zamani wa  Timu ya Taifa ya Tanzania Taifa 
Stars Peter Tino ambaye alifunga goli moja lililoipeleka Tanzania kwa 
mara ya kwanza katika michuano ya AFCON mwaka 1980 iliyofanyika nchini 
Nigeria. Pia Rais Dkt. Magufuli amemsaidia mchezaji huyo wa zamani kiasi
 cha Shilingi milioni tano. 
Rais
 wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa 
anapata chakula cha mchana na viongozi pamoja na Wachezaji wa timu ya 
Taifa ya Tanzania Taifa Stars Ikulu jijini Dar es Salaam.
 
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa 
na Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, 
Naibu Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Juliana Shonza, Rais 
wa TFF Walace Karia, Bondia wa Ngumi za kulipwa Hassan Mwakinyo wapili 
kutoka kushoto katika picha ya pamoja na  Wachezaji wa timu ya Taifa ya 
Mpira wa Miguu Taifa Stars ambao walifika Ikulu mara baada ya kufanikiwa
 kufuzu kushiriki Fainali za michuano ya Mataifa ya Africa AFCON baada 
ya kuifunga Timu ya Taifa ya Uganda The Cranes magoli 3-0 jijini Dar es 
Salaam. PICHA  NA IKULU
=======  =========   =========  ==========
Rais
 wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo 
tarehe 25 Machi, 2019 amekutana na kuwapongeza wachezaji wa Timu ya 
Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) kwa kufanikiwa kufuzu kucheza fainali za
 michuano ya soka Barani Afrika kwa mwaka 2019 (AFCON-2019) na pia 
amempongeza bondia Hassan Mwakinyo ambaye juzi alishinda pambano lake 
dhidi ya bondia Sergio Gonzalez wa Argentina lililofanyika Jijini 
Nairobi nchini Kenya.
Hafla
 ya kuwapongeza wanamichezo hao imefanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam na
 kuhudhuriwa na Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu 
Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, Viongozi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu 
nchini (TFF), Kamisheni ya Ngumi Tanzania (TPBRC) na Kamati ya Ushindi 
ya Taifa Stars iliyoongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Paul 
Makonda.
Akizungumza
 katika hafla hiyo Mhe. Rais Magufuli ameelezea kufurahishwa kwake na 
matokeo ya mchezo wa jana ambapo Taifa Stars iliifunga Timu ya Taifa ya 
Uganda (The Cranes) katika uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam kwa 
magoli 3-0 na ameahidi kuwa Serikali itaendelea kuunga mkono juhudi za 
wanamichezo wote kwa kuwa mafanikio yao yanaliletea Taifa sifa na 
heshima na pia yanatangaza fursa mbalimbali ikiwemo utalii, biashara na 
uwekezaji.
Mhe.
 Rais Magufuli amewapongeza wachezaji wa Taifa Stars, viongozi wa TFF, 
Kamati ya Ushindi ya Taifa Stars na Watanzania wote kwa kuungana pamoja 
kuishangilia timu yao katika mchezo wa jana bila kujali tofauti zao za 
kidini, itikadi za kisiasa, makabila na kanda wanazotoka.
“Kwa
 kweli jana nilifurahi sana jinsi mlivyokuwa mnacheza na jinsi 
mlivyofunga magoli, Watanzania wanataka furaha, sio kufungwafungwa kama 
mlivyofungwa kule Lesotho, ile iliniuma sana hadi nilipanga kuwa sitaita
 tena timu kuja hapa Ikulu, lakini sasa safi.
Nataka
 niwahakikishie Serikali ipo na nyinyi na ni matarajio yangu kuwa 
mtajiandaa vizuri ili mkafanye vizuri katika michuano ya AFCON huko 
Misri, sasa vita imeanza” amesema Mhe. Rais Magufuli.
Mhe.
 Rais Magufuli ametoa changamoto kwa wadau wote wa michezo kuhakikisha 
wanasimamia uboreshaji wa miundombinu ya michezo, wanajipanga vizuri kwa
 michezo mbalimbali ya kuiwakilisha nchi, wanarekebisha dosari zote 
zilizosababisha kusuasua kwa Tanzania katika michezo ya kimataifa na 
ameipongeza TFF kwa kufanikiwa kurejesha mgao wa fedha za maendeleo 
kutoka Shirikisho la Soka Duniani (FIFA).
Aidha,
 ameiagiza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kufuatilia 
uendeshaji wa uwanja wa Taifa ili kujiridhisha juu ya mapato na matumizi
 ya fedha za uwanja huo pamoja na kuangalia ubora wake kutokana na 
kuwepo kwa taarifa kuwa maeneo yanayoharibika hayafanyiwi matengenezo 
inavyopaswa.
Mhe.
 Rais Magufuli amempongeza bondia Hassan Mwakinyo kwa ushindi alioupata 
hapo juzi baada ya kumpiga kwa knockout bondia Sergio Gonzalez wa 
Argentina katika pambano lisilo la ubingwa lilifanyika Jijini Nairobi 
nchini Kenya, pamoja na mapambano mengine ambayo alishinda na amemtaka 
kuendelea kufanya vizuri katika mapambano mengine ili kuipatia sifa 
Tanzania.
“Nafahamu
 kuwa unazo changamoto nyingi ambazo hukusema hapa, lakini nakupongeza 
sana, juzi umemtandika yule jamaa mpaka akakaa chini na huwa nakuona 
unavyofanya mazoezi makali kwa kutumia matairi, wewe ni kijana safi 
sana” amesema Mhe. Rais Magufuli.
Mhe.
 Rais Magufuli ameipongeza kampuni ya Serengeti Breweries Limited ambayo
 ni wadhamini wa timu ya Taifa Stars na SportPesa ambao ni wadhamini wa 
bondia Hassan Mwakinyo kwa mchango wao mkubwa wa kuendeleza michezo.
Katika
 hafla hiyo Mhe. Rais Magufuli amekubali maombi yaliyotolewa na Wizara 
ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ya kusaidiwa maandalizi ya 
michuano ya AFCON kwa vijana wa chini ya miaka 17 iliyopangwa kuanza 
tarehe 14 Aprili, 2019 hadi tarehe 28 Aprili, 2019 Jijini Dar es Salaam 
huku Tanzania ikiwakilishwa na timu ya Serengeti Boys, ambapo amesema 
Serikali itatoa shilingi Bilioni 1 kusaidia maandalizi hayo.
Halikadhalika
 Mhe. Rais Magufuli ametoa zawadi ya kiwanja kimoja cha kujenga nyumba 
Jijini Dodoma kwa kwa kila mchezaji wa Taifa Stars, Bondia Hassan 
Mwakinyo, mchezaji wa zamani na Nahodha wa Taifa Stars  Leodgar Tenga na
 mchezaji wa zamani na mfungaji wa bao lililoiwezesha Tanzania kucheza 
robo fainali ya AFCON mwaka 1980 Peter Tino ambaye pia amezawadiwa 
shilingi Milioni 5.
Kwa
 upande wao wachezaji wa Taifa Stars ambao wameongozwa na Nahodha 
Msaidizi Himid Mao na bondia Hassan Mwakinyo wamemshukuru Mhe. Rais 
Magufuli na Serikali kwa ushirikiano mkubwa walioupata hadi kufikia 
mafanikio hayo na wamemuahidi kuendelea kufanya vizuri katika michezo 
inayofuata.
Rais
 wa TFF Bw. Wallace Karia na Mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa 
(BMT) Bw. Leodgar Tenga wamesema baada ya kufuzu kucheza fainali za 
AFCON sasa Taifa Stars inaelekeza nguvu zake kujiandaa na michuano hiyo 
mikubwa Barani Afrika na pia wameelezea matumaini makubwa ya Tanzania 
kufanya vizuri katika michuano ya AFCON kwa vijana wa chini ya miaka 17 
ambapo Tanzania itawakilishwa na timu ya Serengeti Boys, michuano ya 
AFCON kwa wanawake ambapo Tanzania inawakilishwa na Twiga Stars na 
kufanya vizuri kwa timu ya Taifa ya Soka chini ya miaka 20 (Ngorongoro 
Heros) ambayo tarehe 31 Machi, 2019 itacheza na Eritrea Mjini Asmara. 
Pamoja
 na kuwapongeza wachezaji wa Taifa Stars na Bondia Hassan Mwakinyo Mhe. 
Rais Magufuli amekula chakula cha mchana na wachezaji hao. 
Gerson Msigwa 
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU 
Dar es Salaam 
25 Machi, 2019




















 
No comments:
Post a Comment