Matokeo chanyA+ online




Monday, March 23, 2020

PIKIPIKI 28 ZAKABIDHIWA KWA MAAFISA TARAFA MKOA WA DODOMA

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt Binilith Mahenge amekabidhi pikipiki 28 kwa maafisa tarafa wa mkoa huo huku akiwatahadharisha kutothubutu kuzitumia kwa biashara ya Bodaboda.

Pikipiki hizo ni miongoni mwa pikipiki 448 zilizonunuliwa na serikali kwa gharama ya sh bilioni moja na kugaiwa kwa maafisa tarafa nchini.
Baadhi ya pikipiki zilizotolewa na serikali kwa ajili ya maafisa tarafa
Akikabidhi pikipiki hizo Machi 21 kwa Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini Patrobas Katambi kwa niaba ya Wakuu wa Wilaya wa mkoa huo,Dkt Mahenge amesema serikali imejitahidi kuondoa changamoto ya usafiri iliyokuwepo awali hivyo matarajio yake  ni kuona utendaji kazi unaenda kuimarika na sio vinginevyo.

“Maelekezo yangu kwenu, hizi ni pikipiki ni za kazi za Serikali, sio pikipiki za bodaboda, matokeo yake tunatarajia kuona Maafisa Tarafa mnafika kwenye maeneo yenu yote na kuwasilisha taarifa ya kazi mbalimbali kwenye maeneo yenu na kusimamia utoaji wa huduma za kijamii, kiuchumi na kiutawala.”alisema Dkt. Mahenge.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt Binilith Mahenge akiwa nje ya ofisi yake pamoja na Katibu Tawala wa Mkoa huo Maduka Kessy na Mkuu wa wilaya ya Dodoma Mjini Patrobas katambi wakati wa makabidhiano ya pikipiki kwa ajili ya maafisa tarafa
Amemuagiza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma Gilles Muroto, kuwaelekeza Wakuu wa Polisi wa Wilaya zote mkoani humo kuwakamata na kuwachukulia hatua za kisheria Maafisa Tarafa wote watakao zitumia pikipiki hizo za kwa kufanyia biashara binafsi badala ya kuzitumia kuwafikia wananchi kwenye maeneo yote ya Tarafa zao.

Dkt Mahenge amesema serikali imefanya mengi kwenye sekta za afya, miundombinu ya barabara, viwanja vya ndege,sekta ya anga, reli, usafiri wa majini, nishati, madini, elimu, ukusanyaji mapato na sasa katika kuboresha utendaji wa serikali.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt Binilith Mahenge akimkabidhi pikipiki Mkuu wa wilaya ya Dodoma Mjini Patrobas Katambi kwa ajili ya maafisa tarafa wa mkoa huo
"Tunaona serikali imeimarisha utendaji kazi wa Maafisa Tarafa ambao ni kiungo muhimu kwa kuwawezesha usafiri wa pikipiki,hili ni jambo kubwa sana,"aliongeza.


Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma Kessy Maduka amesema Mkoa wa Dodoma una jumla ya Tarafa 28 na pikipiki hizo zinaenda kuimarisha uwezo wa kuwafikia wananchi wote kwenye maeneo yao na kuongeza ufanisi katika kusimamia shughuli za serikali.


Akipokea Pikipiki hizo Katambi amesema changamoto kubwa iliyokuwa inawakabili Maafisa Tarafa katika kusimamia na kutekeleza shughuli za Serikali kwenye ngazi za Tarafa ilikuwa ni ukosefu wa Usafiri.


"Ndugu zangu niwaombe mkatunze vitendea kazi hivi,sitegemei kuona siku mbili vyombo hivi vimeharibika,"alisema Katambi.


Akishukuru kwa niaba ya Maafisa Tarafa wote Mkoani Dodoma,Afisa Tarafa wa Zuzu jijini Dodoma  Lucas Mbise amesema pikipiki hizo ni ahadi ya  Rais Magufuli aliyoitoa Juni 4, 2019 alipokutana nao Ikulu Jijini Dar es Salaam.


"Mheshimiwa Rais alituahidi na kupitia serikali yake ametekeleza,tunamshukuru sana na tumuahidi kuchapa kazi kama kauli mbiu yake inavyosema ya hapa kazi tu,"alisema Mbise.

No comments:

Post a Comment