Matokeo chanyA+ online




Sunday, April 5, 2020

WAZIRI KALEMANI ATAKA WAKANDARASI KUTUMIA NJIA YA RELI KUSAFIRISHA MIZIGO MRADI WA KUFUA UMEME WA JULIUS NYERERE

Transfoma kubwa iliyopo katika Kituo cha Kupoza Umeme Msamvu mkoani Morogoro. Taswira hii ilichukuliwa Aprili 4, 2020 wakati Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (hayupo pichani) alipotembelea kituo hicho.

 Veronica Simba – Morogoro


Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani amefanya ziara ya kushtukiza katika kituo cha kupoza umeme Msamvu na kuagiza kazi ya kufunga kifaa cha kukata umeme (circuit breaker), ikamilishwe ndani ya siku moja ili wananchi waendelee kupata huduma ya umeme.

Alifanya ziara hiyo jana Jumamosi ya Aprili 4, mwaka huu akiwa ameambatana na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Dkt Tito Mwinuka, Meneja wa Mkoa wa Shirika hilo, Mhandisi FedGrace Shuma, Mwakilishi wa Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Ahmed Chinemba na wataalamu mbalimbali kutoka wizarani, TANESCO na Wakala wa Nishati Vijijini (REA). 
Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (katikati), akimsikiliza Msimamizi wa Kituo cha Kupoza Umeme Msamvu mkoani Morogoro, Selemani Ibwe (kulia) aliyekuwa akimpatia maelezo kuhusu hali ya kituo hicho. Waziri alitembelea kituo hicho Aprili 4 mwaka huu.

Dkt Kalemani alitoa maagizo hayo baada ya kujulishwa kuwa changamoto ya kukatika umeme mara kwa mara ambayo wamekuwa wakiipata wananchi wa mji wa Morogoro hususan maeneo ya Mtibwa na Kilosa ni kutokana na kuharibika kwa kifaa hicho kituoni hapo hali inayowalazimu TANESCO kufunga kifaa kipya.

Waziri alitoa onyo kwa Msimamizi wa Kituo hicho, Selemani Ibwe, kuwa kosa hilo lisitokee tena kwani tayari alikwishalitolea maelekezo kwa Mameneja wa TANESCO nchi nzima.

“Hili ni onyo la mwisho kwa Mameneja wa TANESCO nchi nzima. Mnatakiwa kuhakikisha mnakuwa na vifaa vya akiba katika vituo vya kupoza umeme ili inapotokea hitilafu tatizo linarekebishwa mara moja badala ya kutumia muda mrefu na kuwasababishia kero wananchi.”

Aidha, Waziri alitoa muda wa siku saba kwa wafanyakazi wawili wanaosimamia kituo hicho cha Msamvu kuhamishia makazi yao maeneo ya jirani ili waweze kushughulikia kwa wakati changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika kituo hicho.

Alisisitiza kuwa hilo pia ni onyo la mwisho kwani alikwishatoa maelekezo husika kwa watumishi wote wanaosimamia vituo vya kupoza umeme nchi nzima, kuishi katika maeneo yaliyo jirani na vituo hivyo.

Pia, Dkt Kalemani alitoa maagizo kwa uongozi wa TANESCO mkoani Morogoro kukamilisha marekebisho yanayofanyika katika njia ya kusafirisha umeme ya Mtibwa ndani ya siku tatu ili wananchi husika waendelee kupata huduma ya nishati hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari kituoni hapo, Waziri Kalemani alifafanua kuwa hali ya kukatika kwa umeme ambayo imekuwa ikitokea haisababishwi na ukosefu wa nishati hiyo bali ni kutokana na changamoto za ki-usimamizi ambazo alisema ametoa maelekezo namna ya kuzitatua.

“Mathalani hapa Morogoro umeme uliopo ni wa kutosha kwani kituo hiki kina uwezo wa kuzalisha megawati 88 wakati mahitaji ya wananchi ni megawati 48 tu,” alifafanua.

Awali, kabla ya kutembelea kituo hicho, Waziri Kalemani alizungumza na waandishi wa habari akiwa katika eneo la Dakawa, takribani kilomita 100 kutoka eneo kunapotekelezwa mradi wa kufua umeme wa maji wa Julius Nyerere (megawati 2,115) ambapo alitoa maagizo kwa wakandarasi wa Mradi huo kutumia usafiri wa Reli katika kusafirisha mizigo badala ya kutegemea njia ya barabara pekee.

Huku akiwa amezingatia miongozo ya wataalamu kuhusu kutoweka mikusanyiko ya watu, Waziri alisema maelekezo hayo aliyoyatoa ni kutokana na uharibifu wa barabara husika ambao umesababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha.

“Naipongeza Serikali kwani imejenga miundombinu mbalimbali tunayoweza kuitumia ikiwemo reli ya TAZARA badala ya kutegemea barabara pekee hali inayoweza kusababisha ucheleweshaji wa mradi.”

Akisisitiza, alisema Serikali haitakubali kuona Mradi huo unacheleweshwa kwa kisingizio chochote hivyo akawataka wakandarasi husika kuendelea kuchapa kazi.

Akieleza zaidi, alisema hata yeyé msafara wake umekwama mahala hapo akiwa njiani kwenda kukagua Mradi huo lakini akasema atatumia njia mbadala kufika eneo la Mradi siku inayofuata.

Mkuu wa Wilaya ya Morogoro Regina Chonjo ambaye alifuatana na Waziri Kalemani, alisema amewasiliana na watendaji kutoka Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) ambao ndiyo wenye dhamana na barabara hiyo na kwamba wanatarajiwa kufika eneo husika kwa ajili ya kurekebisha kipande hicho ili kuwezesha magari kuendelea kupita.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Dkt Tito Mwinuka alisema shirika lake litashirikiana na TANROADS katika kuhakikisha njia hiyo inakarabatiwa mapema na kuongeza kuwa hata Mkandarasi anayetekeleza Mradi wa Julius Nyerere atashirikishwa maana pia anawajibika kuchangia.

No comments:

Post a Comment