Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imeendelea kutumia mkakati madhubuti wa nguzo kuu nne katika vita dhidi ya dawa za kulevya nchini. Nguzo hizo ni: (i) Kupunguza upatikanaji wa dawa za kulevya; (ii) Kupunguza uhitaji wa matumizi ya dawa hizo; (iii) Kudhibiti madhara yatokanayo na matumizi; na (iv) Kuimarisha ushirikiano wa kitaifa na kimataifa.
Kupitia mikakati hiyo, katika mwaka 2024 pekee, DCEA imefanikiwa kukamata jumla ya kilo 2,327,983.8 za dawa za kulevya, zikiwemo bangi, mirungi, heroin, cocaine, metamphetamine, hashish, dawa tiba zenye asili ya kulevya na skanka. Mafanikio haya yanatokana na operesheni maalum, doria, na mashirikiano baina ya vyombo vya ulinzi na usalama.
Kwa kushirikiana na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka na Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, jumla ya mashauri 2,785 yaliwasilishwa mahakamani ambapo mashauri 2,021 yalishinda, sawa na asilimia 72 ya mafanikio. TAKUKURU nayo imekuwa kiungo muhimu kwa kuziba mianya ya rushwa katika mfumo wa udhibiti wa dawa hizo, wakati Jeshi la Polisi linaendelea na operesheni za mara kwa mara na kampeni za uelimishaji kwa jamii.
Kwa ujumla, mafanikio haya yanadhihirisha dhamira ya dhati ya serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan katika kulinda afya, usalama na ustawi wa Watanzania dhidi ya athari za dawa za kulevya.
No comments:
Post a Comment