Maadhimisho
ya siku ya UKIMWI Duniani yamezinduliwa kitaifa mkoani Kilimanjaro na Mkuu wa
mkoa wa Kilimanjaro Dkt. Anna Mghwira na kusema kuwa lengo la maadhimisho haya ni sehemu ya kuwakumbuka wapendwa wetu
waliotangulia mbele za haki kwa sababu ya ugonjwa wa UKIMWI.
Akizungumza
katika uzinduzi wa maadhimisho hayo Dkt Anna Mghira amesema kuwa kuanzia leo
hadi Disemba mosi huduma za afya mbali mbali zitakuwa zinatolewa bila malipo
katika viwanja vya Mandela kata ya Pasua manispaa ya Moshi.
Amewahimiza
wakazi wa Mkoa wa Kilimanjaro na mikoa ya jirani kutochesea fursa walioipata
kwani afya ni uhai, ameongeza kuwa mkoa wetu wa Kilimanjaro umepata fursa ya
kuwa mwenyeji katika maadhimisho ya mwaka huu ambayo yanabebwa na kauli mbiu
isemayo “Mshikamano wa Kimataifa-
Tuwajibike kwa Pamoja. “nitafurahi kuona uwanja huu unajaa kila siku kwa
ajili ya kupata huduma na ushauri wa kiafya unaotolewa hapa’ alisema Anna
Mghira.
Uzinduzi
huo ulitanguliwa na matembezi ya hisani kwa ajili ya kutangaza na kuhamasisha
uchangiaji wa Mfuko wa udhamini wa kudhibiti UKIMWI-(AIDS TRUST FUND)
Akizungumzia
umuhimu wa Mfuko wa udhamini wa Kudhibiti UKIMWI (ATF)alisema kuwa Mfuko huu ni
muhimu katika kukabiliana na upungufu wa rasilimali za udhibiti UKIMWI pamoja
na kupunguza utegemezi kwa wahisani, nawaomba wananchi wenzangu tuchangie mfuko
huu kupitia namba ya airtel money 0684 90
90 90 uchangiaji huu uwe endelevu tushikamane tuwajibike kwa pamoja.
Amefafanua
kuwa takwimu zinaonyesha kuwa vijana wenye umri wa miaka 15-24 ndio
wanaochangia asilimia 40 ya maambukizi mapya, hivyo kupitia maadhimisho haya
vijana wataweza kupata elimu sahihi na njia za kujikinga dhidi ya maambukizi
mapya ya VVU kupitia kijiji cha vijana ambacho kitakuwepo kwenye uwanja wa
maadhimisho.
Aidha
kutakuwa na mdahalo wa wanavyuo wenye
lengo la kubadilishana uzoefu wa namna ya kujikinga na maabmukizi mapya ya VVU
katika mazingira ya vyuoni na nje ya vyuo ambalo litawahusisha vijana.
Ameongeza
kuwa Kutakuwa na kongamano kubwa la kisayansi litakalohusu masuala ya UKIMWI
litakalofanyika kwa muda wa siku mbili Novemba 26-27 ambapo katika kongamano
hilo wataalamu watajadili mafanikio, changamoto na namna ya kukabiliana na
changamoto hizo katika kudhibiti maambukizi mapya ya VVU.
Amezitaja
huduma zinazopatikana uwanjani hapo bila malipo kuwa ni pamoja na upimaji wa
hiari VVU,uchunguzi wa kifua kikuu, kisukari, shinikizo la damu, saratani ya
shingo ya kizazi na uwiano wa uzito na urefu.
Amesisitiza
kuwa hamasa ya upimaji wa hiari VVU inawalenga watanzania wote kutambua hali zao
za maambukizi ya VVU, hususani vijana wenye umri wa miaka 15-24 na watu wa
makundi maalum walio kwenye hatari zaidi ya kuambukiza au kuambukizwa VVU wakiwemo
wanaojihusisha na biashara ya ngono na majidunga.
“Natoa
msisitizo kwa wanaume kujitokeza kwa wingi katika kupima ili kujua hali za
maambukizi kwa sababu takwimu za upimaji wa kawaida zinaonyesha idadi ndogo ya
45% ya wanaume hujitokeza kupima VVU, kwa sababu wanaume wengi hutafsiri majibu
ya vipimo vya wenzi wao kwamba ndio majibu yao badala ya wao kwenda kupima”.
Nitoe
rai kwa wananchi kujitokeza katika kupima ambapo watakaogundulika kuwa na VVU
watapata ushauri nasaha na kuanza kutumia dawa za ARV mapema ambapo kutumia
dawa za ARV huwezesha kufubaza na kuimarisha kinga dhidi ya magonjwa
nyemelezi,wajawazito kupunguza hatari ya kuambukiza watoto pamoja na kupunguza
hatari ya kuambukiza VVU kwa wenzi wa ngono.
Aidha
amezungumzia kiwango cha maambukizi ya VVU katika mkoa wa Kilimanjaro kuwa
yameendelea kupungua kutoka aslimia 7.3 mwaka 2004 hadi asilimia 2.6 mwaka
2017, kiwango hiki kipo chini ya wastani wa maambukizi ya kitaifa ambacho ni
asilimia 4.8
Japokuwa
kiwango cha maambukizi kwa mkoa wetu wa Kilimanjaro kipo chini ya wastani wa
Kitaifa haimaanishi kuwa tuko salama hivyo kwa pamoja tunapaswa kuongeza juhudi
ili tufikie lengo la maambukizi sifuri ifikapo mwaka 2030.
Kwa
mujibu wa utafiti huu kiwango cha kufubaa kwa VVU kwa mkoa wa Kilimanjaro ni
asiimia 67 dhidi ya asilimia 52 ya kitaifa hivyo matokeo haya yameuweka mkoa wa
Kilimanjaro kuwa wa pili kitaifa kwa kuwa na kiwango cha juu cha kufubaa kwa
VVU ukitanguliwa na mkoa wa Lindi.
Changamoto
kubwa kwa mkoa wa Kilimanjaro katika kudhibiti maambukizi mapya ya VVU ni
huduma ya tiba na matunzo ambapo baadhi ya WAVIU kutokuwa na ufuasi mzuri wa
dawa za ARV pindi afya zao zinapoonekana kuimarika.
Natoa
rai kwa WAVIU wote waliokwisha anza kutumia dawa za ARV, wazingatie ufuasi
mzuri wa dawa,nawaagiza wadau wote mhakikishe mnawashirikisha vyema WAVIU hasa
waliojiweka wazi juu ya hali zao katika kuhamasisha
WAVIU wasiokuwa na ufuasi mzuri wa matumizi ya dawa za kufubaza (ARV).
Ametoa
shukrani kwa Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia TACAIDS kuupa mkoa wetu heshima ya
kuwa mwenyeji wa wiki ya maadhimisho ya siku ya UKIMWI Duniani kufanyikia
kitaifa mkoani Kilimanjaro.
Ameahidi
kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wadau pamoja na wafadhili wa ndani na
nje ya katika Mwitikio wa VVU na UKIMWI na kuhakikisha dawa zinaendelea kuwepo
bila kukosekana.
Pia
amewashukuru wadau wote wa maendeleo kwa misaada yao ya kifedha na kitaalamu
katika Mwitikio wa VVU na UKIMWI mkoani zinazoendelea kutolewa katika mkoa wa
Kilimanjaro.
Naye
Mwenyekiti wa Baraza la watu wanaoishi VVU (NACOPHA) ameishukuru serikali kwa
kuendelea kutambua haki za watu wanaoishi na VVU ikiwa ni pamoja na kuendelea
kuwapa huduma stahiki,na uhakika wa dawa za kufubaza VVU(ARV)ni hatua kubwa
katika kuhakikisha tunadhibiti maambukizi mapya na kufikia zero mwaka 2030.
Mkurungezi
Mtendaji wa TACAIDS Dr Leonard Maboko ameushukuru Mkoa wa Kilimanjaro kwa
ushirikiano mkubwa katika kuhakikisha maandalizi ya maadhimisho haya
yanafanikiwa.
Amewaomba
wadau kuendelea kuonesha ushirikiano katika kuhakikisha maadhimisho haya yanaleta
chachu ya mabadiliko katika kudhibiti maambukizi mapya ya VVU pamoja na kutoa
elimu ya VVU na UKIMWI kwa wananchi.
Kilele
cha maadhimisho haya yatahitimishwa Disemba mosi, ambapo Waziri Mkuu wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania Mhe.Kassim Majaliwa atakuwa mgeni rasmi.
Imetolewa na
Kitengo cha mawasiliano Serikalini-TACAIDS