Mkurugenzi wa Shirika la Naweza Tena, Bi. Esther Morris, ameibuka kama sauti ya matumaini kwa wanawake waliokuwa wakijihusisha na biashara ya ukahaba na matumizi ya dawa za kulevya jijini Mwanza. Kupitia mradi wa kutoa Stadi za Maisha, shirika hilo limekuwa likiwasaidia Dada Poa na waraibu wa dawa za kulevya kuachana na maisha hatarishi na kuingia kwenye njia salama ya kujitegemea kiuchumi.
Bi. Morris amesema kuwa shirika hilo linawafuatilia kwa karibu walengwa wake, kuwafundisha maadili, kazi halali, na kuwajenga kisaikolojia ili waweze kurejea katika hali yao ya kawaida. Miongoni mwa miradi inayowasaidia ni pamoja na ajira katika kituo cha kuoshea magari, hatua inayowapa kipato halali na heshima mpya katika jamii.
Aidha, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuwekeza katika kinga na tiba dhidi ya dawa za kulevya. Esther amewataka wadau wote wenye nia ya kusaidia kundi hili kuwasiliana nao kupitia namba 0753 85 85 85, ili kwa pamoja kuendeleza mapinduzi haya ya matumaini.
Kauli mbiu: "Wekeza kwenye Kinga na Tiba dhidi ya dawa za kulevya"