Matokeo chanyA+ online




Tuesday, November 26, 2019

SERIKALI HAINA MZAHA UMEME UTAFIKA KOTE - WAZIRI DKT. KALEMANI

Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (katikati), akizungumza na wananchi wa kijiji cha Musasa, kilichopo wilayani Chato, alipofika kuwasha rasmi umeme, Novemba 23, 2019.

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amesema Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais John Magufuli haina mzaha katika kutekeleza ahadi ilizotoa kwa wananchi na kwamba itafikisha umeme katika vijiji vyote nchini ifikapo mwisho wa Desemba mwaka huu kama ilivyoahidi.

Aliyasema hayo kwa nyakati tofauti, Novemba 23, 2019 wakati akizungumza na wananchi wa vijiji vya Musasa na Mutundu, vilivyopo wilayani Chato, Mkoa wa Geita.
“Nafahamu kiu ya umeme mliyonayo wananchi. Tafadhali muiamini Serikali yenu. Umeme utawafikieni nyote kama tulivyoahidi.”
Diwani wa Kata ya Butengolumasa, wilayani Chato, Jeremia Mswanzali, akitoa neno la shukrani kwa Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (Meza-Kuu, kulia), kwa kuwasha rasmi umeme katika kijiji cha Mutundu, Novemba 23, 2019.

Akitoa mfano kuthibitisha namna serikali inavyochapa kazi ili kutimiza ahadi zake, hususan katika kuwapelekea umeme wananchi; Waziri Kalemani alisema kwa Wilaya ya Chato yenye jumla ya vijiji 115, tayari vijiji 101 vimeunganishwa kutoka vijiji 9 tu vilivyokuwa na nishati hiyo mwaka 2015.

Alisema kuwa dhamira ya serikali ni kuhakikisha vijiji vyote vya Tanzania Bara vikiwemo vya Chato vinakuwa na umeme ifikapo mwisho wa mwezi Desemba mwaka huu.
Aidha, Waziri Kalemani aliwasha umeme katika Zahanati ya Kijiji cha Mutundu, Ofisi ya Serikali ya Mtaa wa Musasa pamoja na Mradi wa Maji katika eneo hilo huku akisisitiza maelekezo ya serikali kuwa kipaumbele cha umeme vijijini ni kwa Taasisi za Umma ili kuziwezesha kutoa huduma bora kwa wananchi.
Kaimu Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Mutundu wilayani Chato, Loice Katologo (kushoto), akimkabidhi Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani, risala iliyoandaliwa na wananchi wa kijiji hicho na kusomwa kwake (Waziri) katika hafla ya kuwasha rasmi umeme katika kijiji hicho, Novemba 23, 2019.
Aliwataka wananchi kulinda miundombinu ya umeme katika maeneo yao kwani kuihujumu kwa namna yoyote ni kinyume cha sheria na ni hatari kwa maisha yao.
Vilevile, aliendelea kusisitiza wananchi waliofikiwa na miundombinu ya umeme katika maeneo yao, kulipia gharama za kuunganishiwa nishati hiyo na waachane na kasumba iliyozoeleka na wengi kuwa wanasubiri nguzo kwani hilo siyo jukumu la mwananchi.
Waziri wa Nishati Dkt Medard Kalemani (katikati), akizungumza na wananchi wa kijiji cha Musasa, kilichopo wilayani Chato, alipofika kuwasha rasmi umeme, Novemba 23, 2019.
Kwa upande wao, viongozi wa vijiji husika akiwemo Diwani wa Kata ya Butengolumasa, Jeremia Mswanzali, walitoa pongezi nyingi kwa Rais Magufuli na Waziri Kalemani kwa jitihada wanazofanya kuwapelekea wananchi wanyonge maendeleo hususan umeme vijijini.Veronica Simba - Geita

No comments:

Post a Comment