Matokeo chanyA+ online




Thursday, March 19, 2020

HOSPITALI YA BENJAMINI MKAPA YAPANDIKIZA FIGO KWA MARA YA KWANZA KWA KUTUMIA WATAALAM WAZAWA

Hospitali ya Benjamini Mkapa (BMH)iliyopo jijini Dodoma imefanikiwa kuandika historia kwa kupandikiza figo kwa mara ya kwanza kwa kutumia madaktari wazawa bila kutegemea wataaalam kutoka nje ya Nchi kama ilivyokuwa awali.

Mwanzoni upandikizaji huo ulikuwa ukifanyika kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dodoma(UDOM) pamoja na wataalam kutoka Tokushukay Medical Corporation nchini Japan.
 
Mtambo wa kisasa wa kuvunja mawe kwenye mfumo wa mkojo bila kutumia upasuaji ambao sasa upo katika Hospitali ya Benjamin Mkapa na huduma hiyo itafanyika hapo kwa mara ya kwanza nchini.


Hatua hiyo ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi(CCM) 2015-2020 iliyoahidi kuimarosha mtandao wa hospitali za Taifa pamoja na huduma za ubingwa wa juu zikiwemo za kuchuja damu na kupandikiza figo kwa wagonjwa wenye matatizo ya figo.

Akizungumza Machi 19 na waandishi wa habari Hospitalini hapo, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali hiyo Dkt Alphonce Chandika amesema madaktari hao wamefanya upasuaji huo kwa mgonjwa wa figo Emanuel Kahigi kutoka mkoani Geita

"Kwa kiasi kikubwa tumetimiza tulichokiahidi kwa watanzania,tangu Tanzania iundwe Machi 3 mwaka huu tumefanya upandikizaji bila kutumia wataalamu kutoka nje na mgonjwa anaendelea vizuri,
Mkurugenzi mtendaji wa hospitali ya Benjamini Mkapa Dkt Alphonce Chandika akizungumza na waandishi wa habari hawapo pichani.

Ameongeza kusema,"Huduma hii inapatikana kwa gharama nafuu,nizishukuru taasisi mbili za Japan zimesaidia kwa kiwango kikubwa kutoa utalaam na kuchangia gharama za kuishi kwa wataalam waliokwenda nchini humo kujifunza upandikizaji figo,"alisema Dkt Chandika.


Kutokana na mafanikio hayo amesema wataangalia namna ya kuanzisha kozi maalum za kujifunza upandikizaji ili kusaidia wataalam wengine wa ndani na wa nchi zingine za jirani.
Baadhi ya manesi na madaktari wa hospitali ya Benjamini Mkapa wakiwa na mgonjwa Emanuel Kahigi kutoka Geita aliyefanyiwa upandikizaji wa figo kwa mara ya kwanza na wataalam wa ndani ya nchi

Dkt Chandika amesema pia kwa mara ya kwanza hapa nchini umefungwa mtambo wa kuvunja mawe kwenye mfumo wa mkojo wenye gharama ya sh bilioni 2.5.


Naye Daktari aliyeshiriki upandikizaji figo kwa mgonjwa huyo ambaye ni Daktari Bingwa wa upasuaji kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma(Udom), Dkt. Masumbuko Mwashambwa amesema upandikizaji  huo ulichukua saa 10 ikilinganishwa na muda unaotumika.

“Tulichukua muda mrefu kutokana na kwamba kwanza ndio mara ya kwanza kufanya wenyewe,niwaombe madaktari hasa wanaohudumia wagonjwa wenye matatizo ya figo wasitumie mshipa wa  Femoral Vein kwa kuwa inasababisha kuleta shida wakati wa upandikizaji,”alishauri Dkt Mwashambwa.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Magonjwa ya Figo, Dkt Kessy Shija amesema kulikuwa na wagonjwa wengi kwenda nje ya nchi lakini serikali imeendelea kuimarisha huduma za kibingwa ili wagonjwa watibiwe nchini.

“Hizi huduma tutafanya mara kwa mara tunaomba wananchi waje kwa sababu sasa upandikizaji figo unapatikana nchini, na tatizo limekuwa kwa wale wanaotoa figo kwa ndugu, naomba niwaambie hakuna tatizo lolote ukitoa huduma kiungo chako kimoja kumsaidia ndugu yako,”alisema.

Akizungumzia kuhusu  mgonjwa aliyepandizwa figo amesema aliugua kwa muda mrefu na hakuwahi kuona mkojo wake kwa miaka mitano lakini sasa amepata.

“Ilikuwa ni ndoto kwake,chukulia miaka mitano bila ya kupata mkojo,halafu unakuja kupata kwa kweli ilikuwa furaha kwake,”alisema.

No comments:

Post a Comment