Matokeo chanyA+ online




Friday, February 26, 2021

TANESCO FANYENI VIKAO VYA MARA KWA MARA NA WAFANYAKAZI WENU

 


Naibu Waziri Wa Nishati, Wakili Stephen Byabato ameliagiza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kufanya vikao vya mara kwa mara na wafanyakazi wa shirika hilo kwa kila Kitengo na Idara husika ili kusikiliza changamoto zinazowakabili watumishi hao.

Wakili Byabato alisema hayo, wakati akizungumza na wafanyakazi wa shirika hilo mkoani Simiyu Februari 25, 2021, wakati wa ziara yake mkoani humo.

Alisema vikao hivyo vihusishe wafanyakazi wote bila kujali viwango vya elimu na ngazi za madaraja walizonazo, ili kila mtumishi aweze kueleza yanayomsibu sehemu za kazi pamoja na kueleza namna bora ya kuboresha utendaji kazi wao.


Aliwaeleza kwamba vikao hivyo ndivyo vinavyowafanya wafanyakazi kujiona wao ni sehemu ya familia ya shirika kwa kuwa wanapata muda wa kukaa pamoja na kuzungumza na viongozi wao.

Aidha alitaka watumishi hao kupewa nafasi ya kutoa maoni au mapendekezo yao ya nini kifanyike ili kuboresha utendaji kazi wao pamoja na shirika kwa jumla na maoni hayo yasikilizwe na kufanyiwa kazi.

“Mfanyakazi hutumia muda mwingi wa maisha yake sehemu ya kazi, eneo hili ni muhimu sana kwa kuwa wote hujiona ni familia moja licha ya kila mmoja kutekeleza majukumu yake, hivyo ni muhimu viongozi wa eneo husika kuweka utaratibu kuwa na vikao vya pamoja ili waweze kueleza changamoto zao, na zifanyiwe kazi kwa wakati sahihi, hii inaongeza morali ya kufanya kazi muda wote kwa kasi, ubunifu na usahihi, na katika vikao hivyo mara nyingi hupatikana mawazo chanya ya kujenga na kuimarisha zaidi ubora wa shirika”, alisema Wakili Byabato.


Katika hatua nyingine aliwaonya watumishi hao kufika kazini wakiwa wamelewa ama kunya pombe muda wa kazi, na atakayebainika kuwa na tabia hiyo achukuliwe hatua za kinidhamu kwa mujibu wa sheria za kazi.

Hata hivyo alipongeza wafanyakazi wa shirika hilo mkoani humo kuwa wamekuwa wakifanya kazi zao kwa umakini na kutoa huduma nzuri kwa wateja licha ya changamoto mbalimbali zinazowakabili za kukatika umeme mara kwa mara mkoani humo.

Aidha aliwaeleza kuwa waendelee kuwa wavumilivu  kwakuwa muda si mrefu changamoto hiyo itatuliwa baada ya kukamilika kwa ujenzi wa kituo cha kupoza umeme cha Imalilo.

Kituo hicho kitakuwa na uwezo kuzalisha umeme wa Megawati 90 itakayokuwa ikitumika katika mkoa huo na mikoa jirani, mahitaji ya umeme kwa Simiyu kwa sasa ni Megawati 10 tu.

Mkoa wa Simiyu unapokea umeme kutoka mkoani shinyanga na hivyo kuufanya umeme huo kuwa na nguvu ndogo kuhimili matumizi halisi.

No comments:

Post a Comment